Mhaga: Kwaresima ya Ukarimu


Njia tano za Kuishi Kwaresima hii kwa Ukarimu

Utangulizi

Wapendwa Mahujaji, katika kipindi cha kwaresima, Baba Mtakatifu huwa anatuandikia barua yenye ujumbe maalum kwa ajili ya mfungo wetu. Umuhimu wa funga yetu unaonekana kabisa hata kwa kupitia barua hii. Tunaweza, basi kundonoa mambo baadhi ya kutuongoza katika kuifanya kwaresima yetu iwe karimu kweli.

  1. Sali zaidi, Funga kwa hiari, na Toa Zaidi

“Kwaresima ni musimu wa kuzama zaidi katika maisha yetu ya kiroho kwa njia ya kutakatifuzwa inayotolewa na Kanisa: Kufunga,Kusali na kutoa sadaka.”

Sala, kufunga na kutoa sadaka ni nguzo muhimu katika kukuza imani yetu na katika kuendeleza ukarimu wetu. Mambo ya kawaida kabisa kama kuacha kula nyama, tafakari ya kila siku na nafasi ya kutoa/kuwapa wengine vinapewa umuhimu na KristoYesu mwenyewe (Mt. 6:1-18, 25:31-40). Sali zaidi. Funga kwa hiari yako mwenyewe. Toa zaidi katika kanisa na kwa maskini jirani zako.

  1. Jiweke Huru

“Badala ya kuwa chombo cha kutusaidia kuwatendea mema wengine na kuonyesha mshikamano wetu, fedha inaweza kutufunga na kutufanya tuishi falsafa ya uchoyo inayoondoa nafasi ya upendo na kuzuia amani.”

Kwaresima inatupa fursa ya kutafakari vifungo vya maisha yetu vinavyotuweka mbali na jirani, iwe ni hiyo hela, au mazoeza mabaya au jambo lingine lolote. Kutoa sadaka na kuwapa maskini ni nafasi mwafaka kabisa ya kutusaidia kufungua vifungo vyetu na kuwajengea maisha bora wengine waliodhaifu zaidi katika familia ya watu. Toa sadaka. Wape maskini (Luka 16:19-31). Ubahili, uchoyo, na uroho ni vifungo hasi katika maisha. Kwa kutoa zaidi, unajiweka huru!

  1. Neno ni Taa ya Miguu yako

“Neno la Mungu linatusaidia kufungua macho yetu ili kupokea na kupenda uhai, haswa unapokuwa dhaifu na legevu. Lakini hili kufanya hivyo, inatubidi kuchukulia kwa uzito tunachoambiwa na Injili kuhusu yule mtu tajiri.”

Katika parokia yetu, tuna fursa nyingi za majitoleo kila mtu kulingana na nafasi yake. Na bado, fursa zilizopo za kuzama zaidi katika tafakari ya Neno la Mungu ni nyingi zaidi. Kila simulizi tunayopata ya maisha yaliyojaa matatizo na mahangaiko ya ndugu zetu, tunapewa “neno hai” la kutafakari. Tena, kila mtoto au mtu mzima anayesimulia maisha yake ya ushindi dhidi ya udhaifu na mapungufu yoyote anatupa sisi “Somo la imani” hai kabisa. Kusoma Neno katika jumuiya na kushirikishana neno hilo, kuimarishana katika maisha kwa kufarijiana, na zaidi kuliishi neno hilo ndiyo haswa matendo ya kwaresima. Hija na mafungo, sala za mtu mmoja mmoja na maungamo, vyote hivi vinatusaidia kuzama zaidi katika kiini cha kwaresima. Neno ni taa ya miguu yako(Zab. 119:105)!

  1. Imarisha uhusiano wako na Kristo, Kanisa lake na Jirani yako!

“Kwaresima ni kipindi mwafaka kabisa cha kupyaisha makutano yetu na Kristo, aliye hai katika Neno, katika sakramenti na katika jirani zetu.”

Kila kwaresima tunachochewa na kupewa changamoto ya kuimarisha uhusiano wetu na Kristo, kuja kumjua vyema zaidi—mateso yake, furaha yake na mialiko yake. Njia mojawapo katika mapokea ya kanisa ni kutembea naye kuelekea Kalvario katika vituo vya Njia ya Msalaba. Ni kumtangaza Kristo Msulibiwa, wokovu wetu (1 Kor. 1:23).

Kushiriki kikamilifu katika tafakari ya Njia ya Msalaba ni lishe tosha kabisa ya nafsi zetu katika kujiandaa kupokea kwa upendo na unyenyekevu zawadi ya uhai inayopatikana kwa Kifo na Ufufuko wa Bwana. Sala ya Njia ya Msalaba ni kama utangulizi wa Wiki Kuu na mafumbo yake yote. Shiriki ibada na wengine uimarishe uhusiano wako na Kristo na kanisa lake. Utaweza kumwona Kristo mteseka katika maisha ya wengine na kuchochewa kuwaombea wazima na wafu.  Mt. Yohane Paolo II alifundisha: "Yesu Kristo alifundisha kuwa mwanadamu sio tu kwamba hupokea na kuonja huruma ya Mungu, bali pia anaalikwa kutenda huruma kwa wengine”. Chagua kuvunja miiko yako mwenyewe umwendee jirani yako pawe na upatanisho.

  1. Shiriki katika Utunzaji wa Mazingira

“Nawahamasisha waamini waonyeshe upya wa mioyo yao kwa kushirikishana kampeni ya kwaresima inayopangwa na makanisa sehemu mbalimbali za dunia, na kwa njia hiyo kusaidia katika kukutanisha watu katika familia moja ya binadamu.”
 

Ni juu yetu kuona umuhimu wa kutunza mazingira yetu. Maaskofu katoliki wametoa mwongozo wa Kwaresima ambamo wamesisitiza tuyapende, kuyatunza na kuyaimarisha mazingira yetu (Ebr. 13:17). Kupanda miti, kutunza bustani zetu na kusafisha mazingira tunayoishi ni njia mojawapo mwafaka ya kujihakikishia sisi na ndugu zetu afya ya mwili na roho. Kuweka mazingira yetu safi ni njia ya kutii agizo la zamani zaidi la kuitiisha nchi (Mw.1:28). Shiriki katika utunzaji wa mazingira.

 Tafakari na
Pd. Nicholas Kirimo, SSC


Comments

Popular posts from this blog

TYCS - Muungano wa Mt. Cottolengo (MOCK)

Mwana Mpotevu au Waana Wapotevu?