Mwana Mpotevu au Waana Wapotevu?


Injili ya Kwaresima:
Utangulizi
Nafikiri sio rahisi sana kutoa tafakari kuhusu Mwana Mpotevu. Inaitwa pia Injili ya Baba mwenye huruma. Tutagundua kuwa ina majina zaidi ya haya leo. Mojawapo ya vipengele vinavyovutia zaidi vya Maisha ya Kiroho (mafundisho) ya Mt. Joseph Cottolengo ni msisitizo anaweka katika “Kuwa katika uhusiano mwema na Mungu”. Alitaka ziive kati ya wafuasi wake na Mungu. Na Injili hii (Luka 15:11-32) inatusaidia kutathmini kama tupo sawa. Labda inafaa kufikiria ni wana wawili wapotevu. Hebu tuitafakari pamoja kama Walezi wa Watoto Wa Shirika la Kipapa la Utoto Mtakatifu.
Kupotelewa na Mwana!
Huzuni. Niaminini kweli. Unaweza kuvumilia mara mia kupotelewa na kondoo au hata hela (haya 1-10) kuliko kuvumilia kupotelewa na mtoto. Injili hii utumika mara nyingi kama maandalizi ya maungamo. Inaonyesha picha ya Baba asiyekata tamaa, mwenye huruma kubwa. Hisia tunazopata kuhusiana na tabia ya huyu kijana aliyepotea, na kule kurudi kwake kwa baba, kunaibua maswali lukuki.
Hivi, ule ubavu wa huyu mjinga kumwendea baba na kudai kutaka mgao wake/sehemu yake unavumilika na mzazi kweli? Sio hilo tu, yale majivuno (akatwaa vyote akaenda mbali ugenini... 13) yanavumilika kweli? Kuharibu mali yote katika maisha ya anasa ni ujinga. Lakini ni ujinga zaidi kutaka kurudi nyumbani baada ya kumaliza mali. Ila kwa baba, mwanae amepotea. Hajali mali alizotapanya. Baba hana majuto. Hana hasira. Anatamani mwanaye harudi. Kama anatafuta taarifa, anataka kujua kama yupo hai, kama ana afya. Kama anapeleka salamu, anamtakia mwanae mema, anamwalika harudi. Kila siku anasimama mlangoni na kuangalia kwa subira. Matumaini, huruma, subira... ndizo fadhila zake.
Kurudi kwa Mwana Mpotevu
“Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu... (18). Maamuzi. Mateso yanamfanya mwana akumbuke upendo/ukarimu/wema wa baba yake. Unamtamanisha maisha aliyoacha. Anaamua kurudi. Kurudi kwake ni ishara ya kutubu. Tayari ametubu, amejutia dhambi zake. Hata kama hajui baba atampokea vipi, badala ya kumwogopa baba, anaamua kwenda kwake. Anajiandaa kuungama dhambi zake. Anafanya orodha ya makosa yake.
Kurudi kwake kunaibua sherehe. Kanzu, viatu, ndama aliyenona... ishara za kupokelewa upya, za kurudishiwa hadhi yake/heshima/nafasi yake katika familia. Na Pete? Pete ni ishara ya kuinuliwa zaidi kiheshima. Ni alama ya wazi ya upendeleo wa baba. Kama kanzu tayari ni ishara ya upendeleo (kumbuka Yusufu mwana wa Yakobo?), pete inaonyesha ameinuliwa juu zaidi. Muziki, kucheza, kula na kunywa... karamu kubwa. Baba anaadhimisha kurudi kwa mwanae!
Kurudi kwa Mtoto wa Kwanza
Mzaliwa wake wa kwanza anarudi, anaikaribia nyumba, anasikia vifijo na ngoma. Kwa taarifa yenu, mwanzo wa sura hii, tumeambiwa kuwa watoza ushuru wote na wakosefu walimjia wapate kumsikia. Mafarisayo wakalalamika wakisema, huwapokea wakosefu na anakula nao. Hivyo hii karamu hii ya kumpoka mdhambi aliyerudi inafanana na karamu anazoshiriki Yesu akiwapokea wadhambi waliorudi. Na kumbe wakati watu wakiwa wanakula ndipo Yesu aliwakatisha akaanza kusimulia story hii. Nawaona watu walivyokaa kimya wakimsikiliza. Naona hamu yao ya kusikia ujumbe huu mpya.
Turudi kwa mwanae wa kwanza/mkubwa. Anapopata habari kuwa sherehe hiyo ni kwa ajili ya mdogo wake, ananuna. Aha? Kuna nini? Ni sherehe asiyotarajia. Baba anamwendea. Kama mwanae mdogo alimjia (alimrudia) hapa baba anaenda kumsihi huyu aingie ndani washerehekee. Hebu oneni ilivyo, huyu anakataa kusherehekea kwa sababu anahisi baba hatendi haki. Je, sio hivyo kwetu pia? Sisi nasi hatutamani kuona baba akitenda haki. Namaanisha, amwadhibu mwanae kidogo. Amwonyeshe alichofanya sio sahihi? Aiya! Kurudi hivi hivi ni rahisi akaamua kwenda tena!
Wewe ni nani katika story hii?
Ni rahisi kujiona kama mwana mpotevu. Wakati mwingine kila mmoja wetu anakuwa mwana mpotevu.Nanatamani “kuwa huru”—kutembea anapopenda, kutumia mali ovyo, kujiachia! Kwa nadra sana nakuwa kama baba. Nionyeshe huruma bila kutamani kuadhibu, kukashifu, kukosoa, kueleza? Labda. Lakini bado haijatokea. Inakuwa vigumu kujiona kama mtoto wa kwanza. Huyu anajitokeza zaidi katika maisha yetu. Tunatamani watu waovu wapate adhabu “hili wajirudi”. Kwetu, njia ya msamaha haina uhakika wa kumfanya mkosefu hajirudi kama njia ya adhabu na ukali. Je, unajisikiaje unaposikia hukumu ikitolewa kwa kibaka, mwizi, mhuni? Tunasema haki itendeke!
Oneni jinsi tulivyo wagumu wa kuiga baba yetu? Kweli sisi ni wanae? Tunafanana naye? Nina mashaka sana. Oneni tunavyotamani tutendewe vyema zaidi ya waovu heti kwa sababu tumemtumikia Mungu? Waovu wakipata mema, tunajisikia vibaya. Wakati Neno la Mungu linatuonyesha wazi kuwa mvua yake uwanyeshea wema na waovu sawa. Wakati Yesu ameliongelea tena siku aliposimulia kuhusu wale watu waliokwenda shambani, asubuhi, mchana, jioni na wote wakaripwa denari moja. Kilio cha wale wa kwanza kilikuwa, “Tumefanya kazi zaidi ya hawa waliokuja kazini jioni saa kumi na moja. Tunastahili kutendewa vyema zaidi.” Mbele ya Mungu tunaweza kudai haki kweli? Oneni tulivyo wapendwa!
Hitimisho
Tuvae viatu vya mtoto wa kwanza tuone alivyojikuta katika hali ngumu kumwelewa baba yake. Ni kwaresima. Msishangae. Ni kwaresima wakati tunaposafisha maghala yetu. Mimi nipo bize kufanya usafi kwangu. Sina taimu ya kuangalia kama wengine wapo safi au la. Naamini wapo safi kuliko mimi. Aha! Na kama walezi, tusaidianeni kuwa wema bila kuoneana vivu, bila kujifikiria kuwa wa pekee sana. Tukikumbana na ugumu, tujikumbushie/tukumbushane kuwa sisi ni watoto wa kwanza. Tunatii sheria tu. Upendo wa dhati kwa baba sio mazoea yetu. Hila tunajua kuwa Mungu anatupenda. Hatukati tamaa.
SALA
Ee Mungu mwenyezi, tunakushukuru. Kwaresima ni kipindi cha neema ndani ya mwaka wa kanisa. Ahasante kwa kipindi hiki. Halafu, wewe unayewapenda wanao wote, yule aliyepotelea mbali na huyu aliyepotelea nyumbani, tusaidie na sisi kupendana na kuhurumiana kama wewe unavyotuhurumia. Tupe neema ya kuwa wavumilivu kama wewe ulivyo mvumilivu. Tuwezeshe kuwa karibu na wadhambi hili nao waonje upendo wako. Amina!

“...Mt. Joseph Cottolengo ni msisitizo anaweka katika “Kuwa katika uhusiano mwema na Mungu”.

 

“...Kanzu, viatu, ndama aliyenona... ishara za kupokelewa upya, za kurudishiwa hadhi yake/
heshima/ nafasi yake katika familia..”

 

“...Nionyeshe huruma bila kutamani kuadhibu, kukashifu, kukosoa, kueleza? Labda. Lakini bado haijatokea..”

 



 

 

Comments

  1. Ahsante sana kwa ujumbe mzuri na wenye kuleta tumaini hasa katika kipindi hiki cha Kwaresma. Ubarikiwe!

    ReplyDelete

Post a Comment

Thank you for visiting Bits of the Gospel. We appreciate your comments and support.

Popular posts from this blog

TYCS - Muungano wa Mt. Cottolengo (MOCK)